Friday, December 16, 2011

KUZALIWA KWA YESU MASIHI

KUZALIWA KWA YESU KRISTO

Somo la 18 Luka 1 na 2

Matukio yahusianayo na kuzaliwa kwa Yesu Kristo yameandikwa katika kumbukumbu mbili za Injili. Yanapatikana katika Mathayo 1 na 2 na katika Luka 1 na 2. Luka atwambia kwamba matukio haya yalitokea katika utawala wa Kaizari Augustus (Luka 2:1-2), ambayo inatuwezesha kuthibitisha kwa usahihi kuwa Yesu alizaliwa mwaka wa nne kabla ya Kristo. Injili ya Luka pia imeweka kumbukumbu ya kuzaliwa kwa Yohana Mbatizaji, na kujitokeza kwake katika taifa, ikiweka jambo hili katika sura ya ki-historia pia (Luka 3:1)
Tunapotafakari matukio haya tunafurahishwa na habari kamili zinazotokana na manabii wanaotabiri makusudi ya Mungu ya kumleta Yesu na kazi ambayo angefanya.

Unabii wa Isaya kuhusu kuzaliwa kwa Yesu

Isaya ndiye nabii aliyepeleka ujumbe dhahiri kwa nyumba ya Daudi akisema “Tazama bikira atashika mimba na kuzaa mwana ambaye ataitwa Immanueli (maana yake, ‘Mungu yu nasi’)” (Isaya 7:14). Hili lilitimizwa mara Mariamu, wa ukoo wa Mfalme Daudi alipomzaa mwanawe kifungua mimba Yesu kama alivyotabiriwa katika Mathayo 1:21-23.
Pia Isaya alitabiri kazi ya baadaye ya huyu ambaye angezaliwa akisema: “Kwa maana mtoto amezaliwa kwetu, kuna mwana ambaye tumepewa, na ufalme utakuwa begani kwake. _ _ _ _ kuhusu utawala wake na amani hakutakuwa na mwisho, kwenye kiti cha enzi cha Daudi na juu ya ufalme wake ili kuufanya imara na kuutegemeza kwa njia haki na kwa njia ya uadilifu kuanzia sasa hata milele” Isaya 9:6-7). Kutokana na utabiri huu hatuwezi kushindwa kuelewa kuwa yesu alizaliwa ili atawale katika kiti cha Daudi wakati ufalme wake utakaposimikwa duniani, milele.

Ujumbe wa Malaika Gabrieli kwa Mariamu.

Malaika Gabrieli alipomtokea Mariamu, alimwambia kuhusu kazi maalum ambayo Yesu angefanya. Maneno yake yanamtambulisha Yesu kama uzao wa Daudi uliotabiriwa katika 2 Samweli 7:12-16: “Na tazama utashika mimba na kuzaa mtoto wa kiume ambaye utamwita YESU. Atakuwa mkuu na ataitwa Mwana wa Aliye Juu Zaidi: na Bwana Mungu atampa kiti cha Enzi cha Daudi, baba yake: na atatwala juu ya nyumba ya Yakobo, milele na kuhusu utawala wake hakutakuwa na mwisho (Luka 1:31-33).
Tutafakari maana ya ujumbe wa Malaika Gabrieli kwa Mariamu.
“Utamwita YESU”, Neno Yesu katika Kigiriki ni sawa na neno Yoshua linalopatikana katika Agano la Kale ambalo maana yake ni “Yah (Mungu) ataokoa.” Kupitia Yesu Mungu alikuwa analeta uokovu kutoka kwenye dhambi na mauti kwa watu wote (Linganisha na Mathayo 1:21)
“ataitwa Mwana wa Aliye Juu Zaidi.” Angekuja kuwa “Mwana wa Mungu” aliyeahidiwa kwa Daudi katika 2 Samweli 7:14 (linganisha na Waebrania 1:5; Zaburi 2:7.
“Bwana Mungu atampa kiti cha enzi cha Daudi, baba yake.” Yesu ni “mzao” au mjukuu aliyeahidiwa kwa Daudi ambaye ataanzisha upya kiti cha enzi na ufalme wa Daudi duniani (2 Samweli 7:12-16; linganisha Isaya 9:6-7)
“Kuhusu ufalme wake hakutakuwa na mwisho” ufalme wake hautakuwa na mwisho kwa sababu Yesu Kristo ambaye atkuwa mfalme hafi (2 Samweli 7:16, Danieli 2:44, Ufunuo 11:15).
Katika mbiu fupi ya Malaika Gabrieli tunapata maelezo dhahiri ya kazi itakayofanywa na mtoto huyu ambaye alikuwa karibu kuzaliwa:
 Angewaokoa binadamu katika dhambi na mauti
 Angekuwa Mwana wa Mungu
 Angekuwa mwana wa Daudi, na kwa hiyo
o Angekalia kiti cha enzi cha Daudi
o Angetawala Waisraeli waliojikusanya upya
o Angeanzisha ufalme wa Mungu usio na mwisho duniani.

Jibu la Mariamu kwa mbiu ya Gabrieli lilikuwa la unyenyekevu na ukunjufu kwa matakwa ya Mungu. Aliuliza: “Hili litakuwaje? Maana simjui mwanaume?
Jibu la Gabrieli likawa; “Roho Mtakatifu atakujia na uwezo wa Aliye Juu Zaidi utakufunika: kwa hiyo hicho kitu kitakatifu kitakachozaliwa na wewe kitaitwa Mwana wa Mungu” Luka 1:34). Kupitia uwezo wa Roho Takatifu ya Mungu mtoto huyu angezaliwa na kuitwa “Mwana wa Mungu” kwa utimizo wa unabii wa Agano la kale (2 Samweli 7:14, Zaburi 2:7, angalia Matendo 13:32-33, Mwanzo 3:15).

Kuzaliwa Kwake Bethlehemu

Kuzaliwa kwa Yesu Bethlehemu kulikuwa kumetabiriwa na Nabii Micah (Micah 5:1-2) lakini Yusufu na Mariamu waliishi Nazareti kilometa 110 kaskazini mwa Bethlehemu. Mariamu alikuwa amekaribia kujifungua na katika hali ya kawaida ya kibinadamu ilionekana kwamba angejifungulia Nazareti. Walakini tunaona mkono wa Mungu ukifanya kazi miongoni mwa binadamu, kuonyesha makusudi yake (angalia danieli 4:17), kwa maana wakati huu Kaizari Augustus alitoa amri kwamba dunia nzima ilipe kodi (yaani watu wote waorodheshwe). Hili lililazimu Yusufu na Mariamu wafanye safari ndefu kwenda kwa mji wa babu zao, Bethlehemu kwa madhumuni hayo (Luka 2:1-6) kilichoonekana kama uamuzi wa mbali wa mtawala wa Kipagani, kilikuwa kwa kweli kimeongozwa na mkono wa Mungu katika mashauri ya wanadamu kwa maana Yesu alikuwa azaliwe Bethlehemu (Luka 2:4-7, Mathayo 2:4-6). Pia Micah alitabiri kazi ya baadaye ya Yesu akisema angekuwa “Mtawala Israeli” Hili litatimizwa mpaka mpaka atakaporudi kuja kusimika ufalme wa Mungu duniani.

Habari zenye kufurahisha za kuzaliwa kwake.

Tukio hili lililosubiriwa kwa muda mrefu na vizazi na vizazi vya wacha Mungu wa kuume na kike liltangazwa na malaika kwa wachunga kondoo katika nyanda za Bethlehemu. “Msiogope; kwa maana, tazameni, nawaletea habari njema za furaha kuu kwa watu wote. Kwenu leo hii amezaliwa Mwokozi ambaye ni Kristo Bwana katika mji wa Daudi” (Luka 2:10-11).

Aya ya 10:
“Habari njema” Hii ni tafsiri ya neno lilelile ambalo mahali pengine limeandikwa “Injili”.
“Kwa watu wote” Habari njema inayohusiana na Yesu Kristo Bwana si kwa Wayahudi peke yao bali kwa watu wote, Wayahudi na watu wa mataifa sawia. Hizi habari njema ni mbiu ya uwokovu ambao Mungu ametoa kupitia kwake (Marko 16:15-16, Wagalatia 3:26-27)

Aya ya 11:
“Katika mji wa Daudi” Ndiyo kusema Bethlehemu, mji alipozaliwa Daudi (1 Samueli 16:1) Israeli ilitarajia mtawala ajaye atokee katika mji huu (Micah 5:1-2).
“Mkombozi” Mwanadamu ni mwenye mauti na dhambi na anahitaji kukombolewa kutoka katika kifo. Kupitia kwa Yesu Kristo Mungu ametupatia msamaha wa dhambi na matumaini ya kuchangia kutokufa na kristo wakati atakaporudi duniani (2 Timoteo 1:10; 1 Wakorinto 15:21-23, 51-54) kwa hiyo Yesu ni “Ukombozi wa mwanadamu utokao kwa Mungu.”

Wanajimu Kutoka Mashariki.

Miongoni mwa wale waliokuwa wamesoma unabii na kutarajia kuzaliwa kwa Kristo wakati huo ni “Wanajimu kutoka sehemu za Mashariki.” Mara tu walipofika Yerusalemu walianza kuuliza. “Yuko wapi yule aliyezaliwa akiwa mfalme wa Wayahudi?” (Math. 2:2) walielewa kutokana na Manabii kuwa hatima ya mtoto aliyezaliwa ni kuwa Mfalme wa Wayahudi akikalia kiti cha enzi cha Daudi (2 Samweli 7:12-14; Isaya 9:6-7)
Herode aliposikia udadisi wa Wanajimu alifadhaika na kuita Makuhani na Waandishi na “kuwataka wamwambie ni wapi Kristo alipokuwa amezaliwa” (Math. 2:4), walijua jibu mara moja kutokana na Nabii Micah wakamjibu: katika Bethlehemu ya Yuda (Micah 5:2; Math. 2:5-6).
Kutokana na hili twaona kuwa Wayahudi walifahamu kwamba:
 Kristo angezaliwa
 Katika Bethlehemu
 Na angetawala “watu wangu Israeli.”

Yesu Mwana wa Mungu na Mwana wa Binadamu.

Majina haya mawili, “mwana wa Mungu” na “Mwana wa Binadamu” yanatumika katika kumbukumbu zote za Injili. Yanaonyesha kuwa Mungu alikuwa baba yake na wakati huo huo akiwa mzao wa Adam alihusiana na mwanadamu ambaye yeye alikuja kuokoa. Tunaona hizi nasaha mbili zikitangazwa na Gabrieli katika maneno yake kwa Mariamu. Angekuja kuwa “Mwana wa Aliye Juu Zaidi” yaani wa Mungu na angekalia “kiti cha enzi cha Daudi, baba yake” (Luka 1:32; 2 Samweli 7:12-14; Matendo 2:30).
Paulo asema “Wakati ulipotimia “Mungu alimtuma mwanaye aliyezaliwa na mwanamke katika sheria” (Wagalatia 4:4) kuhusu mwanae Mungu aliweza kusema “Wewe ni mwanangu, leo hii nimekuzaa” (Zaburi 2:7, Waebrania 1:5; 5:5)
Ingawa kuzaliwa kwa Yesu kulibashiriwa muda mrefu na manabii kuwepo kwake kulianza mara Mungu kupitia Roho Yake Takatifu aliposababisha Mariamu kubeba mimba, miaka 2000 iliyopita (Luka 1:35)
Nabii Isaya anataja kuzaliwa kwa Yesu Kristo Bwana kwa jinsi hii: “Na yeye (mungu) aliona kuwa hapakuwa na yeyote, na kuwaza kwamba hapakuwa na mtetezi: kwa hiyo mkono wake ukaleta uwokovu kwake” (Isaya 59:16).

Mungu kwa kuona hali ya dhambi za binadamu na kwa kujua kwamba hapakuwa na yeyote ambaye angeonyesha utii mkamilifu au kumwokoa mwanadamu katika utumwa wa dhambi na mauti, alichukua hatua ya kumpata mtu ambaye kwa kupitia kwake angeleta uokovu. Alimtia nguvu huyo aliyezaliwa na mwanadamu ili ashinde dhambi na mauti na hiyo kufungua njia ya wokovu na uhai kwake mwenyewe na wengine wote ambao wangekuja kwa mungu kupitia kwake, “ kazi ya mwana wa Adamu imeainishwa katika Waebrania 2:6-18.

Ulazima wa mungu kujihusisha na wokovu wa mwanadamu kutoka katika dhambi ulitabiriwa tangu mwanzo, Aliposema “uzao wa mwanamke” ungekiponda kichwa cha “nyoka” kuonyesha kwamba Mungu angemfunika mwanamke kwa kivuli chake ili azae mwana ambaye angevunja nguvu ya dhambi ya nyoka Mwanzo 3:15; Waebrania 2:14, Wagalatia 4:4)

Uhusianao wa Yesu na Baba yake.

Yesu, kwa uangalifu aliueleza uhusiano wake na Baba yake, kila mara akitambua udogo wake kwake katika kila jambo, yesu alisema: “Baba yangu ni mkuu kuliko mimi” “Yoh.14:28 linganisha na Yoh 5:19, 30). Uhusiano huu wa Baba na Mwana ulionyesha umoja au mwafaka katika makusudio yao (Yoh 10:30) Alikuja kutekeleza matakwa ya Baba yake Yoh 5:30; Waeb 10:7) na kwa njia ya kupendeza alionyesha tabia ya Baba (Yoh 14:9)

Uhusiano huu mkuu ulieleweka wazi na kwanza kabisa kuandikwa akiwa na umri wa miaka 12: “Hamjui kwamba ni lazima niwe katika nyumba ya Baba yangu?” Alitambua kuwa Baba yake alikuwa amemlea kwa ajili ya kazi maalum na alikuwa amedhamiria kuifanya. Maisha yake yalikuwa ya kujitoa na utii kwa Baba yake, yakuishia katika mateso na kifo msalabani ambapo watu wangekombolewa katika dhambi na mauti.

Katika uhai wake wote aliweza kusema “Chakula changu ni mimi kufanya mapenzi yake aliyenituma na kumaliza (Yoh 4:34) Na hivyo katika zile saa za mateso kuelekea kutundikwa kwake msalabani aliomba apate nguvu katika bustani ya Gelsemane kwa maneno haya: Baba kama inawezekana, naomba kikombe hiki kinipite; hata hivyo sikulingana na mapenzi yangu lakini kulingana na mapenzi yako. “(Mathayo 26:39) mapenzi ya Baba yake yalikuwa na nguvu zaidi na ilibidi yatimizwe. Mateso yake ya kutisha msalabani yalipokwisha alipaza sauti kwa kuridhika na afueni: “Imekwisha “akainamisha kichwa na kukata roho akijua kuwa kazi yake ilikuwa imekamilishwa (Yoh 19:30) Aliweza kusema “Nimemaliza kazi uliyonipa kufanya” (Yoh 17:4).

Tunapotafakari mapenzi na utii ambao mwana alimfanyia Baba yake wakati wote tunaweza kuelewa kwa nini mungu alibainisha mara mbili: “Huyu ni mwanangu nimpendaye nipendezwaye naye” (Math. 3:17, 17:5)

Kwa heshima, tuelewe kwamba, Yesu, japo mwanaume aliyezaliwa na hulka ya kibinadamu alikuwa pia mwana wa Mungu, ambaye kwa kushinda dhambi na mauti alifufuliwa katika wafu na kupazwa mbinguni na kukalishwa upande wa kulia wa Baba yake.

Ni muhimu kwamba tunaelewa wazi uhusiano wa Baba na Mwanae ili kuifahamu kazi ya Yesu Kristo Bwana wetu. Kukosa kuelewa kumesababisha dhana potofu ya utatu kwamba yesu alikuwa mungu, sawa na wa milele kama Baba. Fundisho kama hilo halipatikani mahali popote katika Biblia, Kuwa ushahidi wa kutosha kabisa kuthibitisha kuwa fundisho hilo ambalo limekuja kuwa la msingi kwa imani za kikristo siku hizi halikuundwa hadi miaka 300 baada ya Kristo.

Maneno yanayotumiwa kwa kawaida na wale wanaoshikilia fundisho la utatu kama, Mungu Mwana “aliyesawa” na mwenye “umilele” na hata Utatu”, hayapatikani mahali popote katika Biblia. Hata wafuasi wa kanisa wanaoheshimika wanatambua kuwa fundisho hilo halimo katika Biblia, lilijengwa kama fundisho la lazima na watu walioongozwa na falsafa ya Kigiriki na kulishushia kwenye mafundisho rahisi ya Biblia. Kwa kuwa inakubalika kuwa hakiwezikueleweka kinaitwa “fumbo”, Na hili limewavunja wengi moyo wa kutafuta ukweli.

Yesu mwenyewe, kwa upande mwingine alisema ni suala la uzima wa milele kumjua Mungu: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli na yule uliyemtuma Yesu Kristo (Yohana 17:3).

Mtume Paulo anaandika juu ya jambo hili kwa uwazi kabisa: kuma Mungu mmoja na mtetezi mmoja kati ya Mungu na wanadamu, Yesu Kristo (I Timotheo 2:5).


Yesu – neno lililogeuzwa kuwa Mtu

Mungu alimtangazia Musa na wana wa Israeli “Nitawainulia nabii kutoka katikati ya ndugu zao kama wewe; nami nitaweka maneno yangu katika kinywa chake, naye atawaambia maneno yote nitakayomwamuru na itatukia kwamba mtu ambaye hatasikiliza maneno yangu ambayo atayasema kwa jina langu mimi mwenyewe nitamtaka ajibu” (kumbukumbu 18:18 – 19, Hapa Mungu anatueleza mapema jinsi atakavyo ingilia kati masuala ya duniani na kumuinua mwana ambaye atamwagiza kunena maneno yake kwa taifa. Kwa kuwa aya hizi zimo katika mfumo wa wakati ujao Yesu, japo alikuwa katika mpango wa Mungu, hakuwepo wakati huo. Kwa kuwa Mungu alimuamuru mwanae kuweka maneno kinywani mwake, Yesu, pia aliitwa “Neno lililofanywa Mtu.
Tunasoma: “Neno lilifanywa Mtu na kuishi miongoni mwetu (na tuliona utukufu wake, utukufu kama wa mwana wa pekee wa Baba) uliojaa neema na ukweli” Yoh.1:14). Neno la Mungu halikuwa jambo la kinadharia tu bali lilokuwa na mwongozo wa kimaadili kwake ili kwamba alionyesha tabia halisi ya Baba yake akiwa amejaa neema na kweli. Hivyo yesu aliweza kumwambia Filipo; “yule aliyeniona mimi amemwana Baba na wewe utasemaje tuonyeshe baba yako?” Yoh. 14:9) Yesu hasemi kuwa yeye ndiye Baba, Anachosema ni “Ninafanya kile Mungu alichotaka nifanye na nina sema kile ambacho mungu amenitaka niseme kama umeniangalia utakuwa umeona kuwa ninewaonyesha tabia ya Baba yangu kwa sababau mimi ni mwanawe na siku zote ninatekeleza mapenzi yake” kabla ya kusulubiwa alimwomba Baba yake akisema “Nimelitambulisha jina lako kwa watu ulionipa duniani” (Yoh. 17:6)

Kila mara Yesu alikiri kuwa maneno aliyo kuwa akisema hayakuwa yake mwenyewe bali aliyofundishwa na Mungu: Sijajisemea Mwenyewe; bali Baba aliyenitumia akinipa amri, ninachotakiwa kusema na ninachopaswa kunena. Na ninajua kuwa amri yake ni uzima wa millele. Chochote ninachosema kwa hiyo ni kile Baba alichoniambia kwa hiyo ninasema (Yoh 12:49-50, 7:17, 8:28) Yesu alisisitiza siku zote kuwa alikuwa Mwana wa Mungu na mdogo kwa Baba yake.
Alisisitiza hivi: “Baba yangu ni Mkuu zaidi kuliko mimi” (Yoh.14:28) Wayahudi waliposema Yesu “anajifanya kuwa hawezi kufanya lolote peke yake,” na tena “Mimi peke yangu siwezi kufanya chochote” Yoh 5:18 – 19, 30)

Uhusiano huu mzuri kati ya Mungu na Mwanae ni wa msingi kueleweka kama tunataka kuamini ukweli. Yesu alisema “Huu ni uzima wa milele kwamba waweze kukujua wewe Mungu pekee wa kweli na Yesu Kristo uliyemtuma (Yoh. 17:3)


Maisha ya Yesu ya awali

Kumbukumbu za injili za twambia machache sana kuhusu maisha ya yesu kwanzia alipozaliwa hadi alipofikisha umri wa miaka 30, wakati alipotambulishwa katika taifa lake kwenye ubatizo wake na Yohana Mbatizaji (Luka 3:23)

Tukio peke yake lililoandikwa ni pale alipoandamana na Yusuf na Mariamu kwenda Yerusalemu kwenye sikukuu ya Pasaka alipokuwa na umri wa miaka 12, hapa tunasoma: “Yesu aliongezeka katika hekima na urefu na katika kupendwa na Mungu pamoja na wanadamu” (Luka 2:41 – 52)


MUHTASARI

 Kuzaliwa kwa Kristo kulikuwa kumetabiriwa na Nabii Isaya (Isaya 7:14; 9:6–7).
 Neno “Yesu” maana yake ni “Mungu (Yah) ataokoa”. Ni Mungu ndiye aliyemtoa Mwanae kwa wokovu wa Wanadamu katika dhambi na mauti (Math 1:21, linganisha na Isaya 45:21 – 22).
 Malaika Gabrieli alimtokea Mariamu na kumwambia kuwa angezaa mwana wa Mungu ambaye pia Mwana wa Daudi (Luka 1:31 – 33; 2 Samweli 7:12 – 14).
 Yesu alizaliwa akiwa yule aliyeahidiwa kukaa kwenye kiti cha Daudi, Yerusalemu mara kitakaporudishwa na atatawala milele (Luka 1:31 – 33, 2 Samweli 7:12 – 16).
 Bethlehemu ni mji ule ambapo Yesu angezaliwa (Micah 5:2, linganisha na Math 2:4 – 6, Luka 2:4 – 11 )
 Tabia ya Mungu ilidhihirishwa katika maisha ya Mwanae (Yoh 14:9,17:6) kwa kuwa siku zote alinena maneno ya Mungu aliitwa Neno lililofanywa mtu Yoh 1:14, Kumbukumbu 18:18 – 19; Yoh 12:49 – 50; 7:17; 8:28)
 Yesu ana tajwa kama “Mwana wa Mungu” Hakuna mahala popote katika Biblia alipotajwa kama “Mungu Mwana” wala hadai kuwa sawa na Mungu au wa milele na Mungu kama mafunzo ya utatu yanavyodai, Siku zote alikiri kuwa Baba yake alikuwa Mkuu kuliko yeye, (Yoh 14:28 Linganisha na 5:18 – 19, 30)

SOMO LA 18 – MASWALI

1. Jina “Yesu” lina maana gani?
2. Maneno ya Malaika Gabrieli yalibashiri nini kuhusu kazi ya Yesu Kristo?
3. Maneno haya yatatimizwa lini?
4. Yesu alizaliwa katika mji gani wa Israeli?
5. Kwa nini Yesu anaitwa Mwana wa Binadamu?
6. Mungu alimsema Yesu “Nitakuwa Baba yake nae atakuwa Mwanangu” (2 Samweli 7:12 – 14 na Waebrania 1:5) Je Yesu alikuwepo kabla ya kuzaliwa na Mariamu huko Bethlehemu?
7. Je Yesu alidhihirishaje Jina la Mungu katika maisha yake?
8. Yesu hakudai kuwa sawa na Mungu katika maisha yake. Nukuu kifungu kinacho sema Baba yake ni Mkuu kuliko yeye.